Pages

Saturday, July 21, 2012

WARAKA KWA MADIWANI WA CCM NA TLP KUHUSU MGOGORO WA MEYA ARUSHA MJINI

WAHESHIMIWA MADIWANI,
CCM NA TLP
HALMASHAURI YA MANISPAA YA ARUSHA

YAH: MGOGORO WA MEYA ARUSHA MJINI

Tafadhali husika na kichwa cha habari hapo juu.
Sisi Madiwani wa CHADEMA tumefikiri na kutafakari kwa kina kuhusu mustakabali wa maendeleo ya wananchi wa Manispaa ya Arusha Mjini. Kwa nafasi yetu ya wawakilishi na utetezi wa wananchi Arusha kwa umoja wetu ni vema tufikiri na tutafakari kwa kina kwa pamoja hasa kipaumebele ikiwa ni kutanguliza HAKI na MAENDELEO katika kumlenga kila mkazi wa aliyepo katika Halmashauri yetu. NI vema tukawa WAKWELI na WAZELENDO kwa wananchi wetu wa Arusha, huku wote tukijua kwa kina kile kilichotokea Arusha.

Kwa muda mrefu kumekuwa na mgogoro wa Uchaguzi wa MEYA wa manispaa ya Arusha, ambayo ilitokana na ukiukwaji wa kanuni na taratibu za uchaguzi wa Meya ambayo akidi yake ilikuwa haijatimia. Ikumbukwe kuwa Mhe. Kivuyo ambaye katika sakata hilo alijikuta akichaguliwa kwa hila kuwa NAIBU MEYA, alifikia hatua ya kujizulu nafasi hiyi na kukiri mbele ya waandishi wa habari na wananchi wa Arusha kuwa uchaguzi uliofanyika haukuwa wa haki na yeye alipewa nafasi hiyo kwa hila, kitu ambacho baada ya tafakari ya kina aliamua kujiuzulu ili asiwe sehemu ya dhambi hiyo na kujikuta anakalia KITI CHA DAMU. Jambo hili pia limekuwa likisemwa na baadhi ya madiwani wa CHAMA CHA MAPINDUZI pindi tunapokutana nao kuwa mfumo wa chama cha CCM unazuia kuyatamka haya lakini ukweli ni kuwa huo uchaguzi wa meya uliofanyika na Mhe Gaudence Lyimo kupata nafasi hiyo ulikuwa batili kwa mujibu wa kanuni, lakini mbaya zaidi, umepelekea damu kumwagika, jambo ambalo ndio baya.

Wote tunashuhudia jinsi ambavyo mgogoro huu ulivyo na madhara makubwa sana kwa wananchi wetu na sisi pia ambao ni sehemu ya jamii hiyo hiyo. Mbali na kusababisha watu watatu kupoteza maisha, pameendelea kutokea sintofahamu kubwa kutoka kwa wananchi jambo ambalo limeendelea kuzidisha hasira kwa wananchi kwa serikali. Jambo hili ni vema likafanyiwa kipimo maana mchezo huu na hila hii inaweza kuzaa balaa ambalo sio rahisi kulimudu tena.

Dharau na makusudi yanayofanywa na chama cha mapinduzi, mathalani Mhe Gaudence Lyimo na MKURUGENZI wa halmashauri katika kupuuzia wito wa CHADEMA kuwa HAKI haikutendeka, KANUNI zilivunjwa na hivyo uchaguzi wa MEYA ufanyike upya kwa kufuata kanuni sasa inafika mahali haivumiliki na hapo ndipo itakuwa mikononi mwa wananchi na sio CHADEMA tena.

Sambamba na hali hii, pia mgogoro huu unatumiwa na watendaji wa Halmashauri kufanya mambo yao yasiyo ya kiuadilifu kwani hakuna udhibiti wa kabisa katika uendeshaji wa halmashauri yetu. Waheshimiwa madiwani, katika ukweli huu, MKURUGENZI na huyo anayeitwa MEYA watatoa wapi ujasiri na kujiamini “moral authority” ili hali wao wameshiriki dhambi mbaya ya kuchakachua kanuni za kufanya uchaguzi wa meya isivyo halali na mbaya zaidi Mhe Gaudence kuendelea kung’ang’ania nafasi hiyo kwa kiwango cha damu ya watu kumwagika bila hata kujali??

Hata hivyo, hata kama Mhe Gaudence Lyimo hatajali wito huu ambao kwetu ni wito wa mwisho kwake na chama chake, jambo hili tunaliacha kwa MUNGU mwenye HAKI atashughulika nae kwa wakati wake na muda si mrefu tutapata majibu ya maombi yetu. Pili tunaliacha jambo hili kwa wananchi ili waamue kwa sababu wameshajua wazi kuwa Mhe Gaudence Lyimo na chama chake waliamua na wameendelea kuwafanyia uhuni katika mji wao. Sisi tumeliacha kwao waamue watakavyoamua.

Tunafahamu kabisa katika nafsi na mioyo yenu mnafahamu uchaguzi haukuwa halali lakini mnashindwa kusimamia ukweli kwa sababu ya ubinafsi na kukosa uzalendo kwa wananchi wa Arusha kwa kutanguliza maslahi yenu mbele, kitu ambacho tusingependa kipewe tafsiri hiyo
Tunawasihi kwa dhati kabisa tuamue kwa pamoja kwa manufaa ya Arusha tukubaliane kama viongozi wazalendo, wapenda maendeleo na wenye hofu ya MUNGU tufanye uchaguzi wa MEYA wa Halmashauri ya Arusha ambao utakuwa ni halali kwa vyama vyote.

Nchi nyingi za Afrika kumekuwa na vita vya wao kwa kwao kwa sababu ya uchu wa madaraka. Hili limetokea pia hapa Arusha watu wamekufa kwa sababu ya MEYA, hii ni aibu na ni dhambi kwa kung’ang’ania madaraka ambayo si haki.

Waheshimiwa madiwani wenzetu hata juhudi za serikali kufanya maendeleo wananchi wengi wa Arusha bado hawana imani na serikali yao kwa sababu ya MEYA tu. Hivi sasa kuna mradi wa ujenzi w barabara unaondelea ukweli ni kwamba jambo hili ni zuri lakini wananchi wanalibeza sana kama vile linafanywa kwa hila. Kwa nini iwe hivi??

Kimsingi tunataka MEYA ambaye yupo huru kutembelea kata zote kwa ajili ya maendeleo bila kujali itikadi ya chama chake. Hatutaki MEYA anayevizia misiba na harambee.
Mwisho tunamwomba Mh. Gaudence Lymo atafakari kwa kina kwa kumuomba MUNGU wake ampe hekima na ujasiri wa kuchukua maamuzi magumu ya kujiuzulu nafasi ya UMEYA na uchaguzi wa kidemokrasia ufanyike kwani utampa heshima na amani katika maisha yake yote.
Tunaomba Waheshimiwa Madiwani wenzetu kwa pamoja tuseme dhambi hii imetosha na tutubu kwa kufanya uchaguzi wa haki na Amani. Na kwa dhati kabisa yeyote atakayechaguliwa hata kama ni Mh. Gaudence tutampa ushirikiano wa dhati kabisa.

Tunaomba ushirikiano wenu katika jambo hili ambalo ni la msingi kwa maendeleo ya watu Arusha. Kila mmoja kwa imani yake aombee jambo hili kwani halitaki ushabiki linahitaji utulivu wa akili.

WAHESHIMIWA MADIWANI, FANYENI TAFAKARI YA KINA, ZINGATIENI JINSI WANANCHI KATIKA KATA ZENU WANAVYOWATAZAMA, ni matumaini yetu kuwa tutafanya uchaguzi wa MEYA ndipo tufanye uchaguzi wa Naibu MEYA. Na jambo hili litakuwa ni ushindi na sifa iliyotukuka kwa MADIWANI WOTE na sio kundi fulani la watu.

Asanteni sana

Doita Isaya Harri
Mwenyekiti madiwani wa CHADEMA

Nakala:
Katibu wa CHADEMA (M)
Katibu wa CCM (M)
Katibu wa TLP (M)
Mkurugenzi wa Halmashauri – Arusha Mjini

Popular Posts